Monday, 10 November 2014

Are you there !!!


Katika mafanikio hakuna muujiza fanya unachofanya(kazi au biashara) kwa bidii kutimiza ndoto zako.

Friday, 31 October 2014

TANGAZO

FURAHIA ZANZIBAR!! Tarehe 07/11/2014. Best Travel Solutions Tumeandaa safari ya kwenda kisiwa cha karafuu kwa siku 3. Gharama za usafiri wa boat, malazi na ada kwenda Prison Island, Spice Farm na Stone Town ni Tsh 225,000/- kwa mtu mmoja (single) au Tsh 390,000/- watu wawili (couple). Wahi sasa nafasi ni chache. Kwa maelezo zaidi piga 0653952515. Karibu sana!

Monday, 4 August 2014

Unataka dili la koboresha maisha yako? soma hapa !!

Angalia jinsi maisha yanavyozidi kuwa magumu katika jamii zetu. Gharama za vyakula, usafiri, na mambo mengine zinazidi kuongezeka, pia mabadiliko ya kiteknolojia na kijamii yanaleta changamoto nyingi. Tupo katika zama ambapo kusimama kiuchumi kunahitaji kujidhatiti kweli kweli. Makala hii inachambua mambo ya msingi ambayo yanaweza kukusaidia kujipanga kupata dili zinazoweza kuinua maisha yako.
1. Jitafakari: 
Ni vizuri kujizoesha kutafakari kuhusu wewe ni nani, mapungufu yako, mambo gani makubwa na mazuri uliyokwisha wahi kufanya, na vitu gani hasa unavipenda na usivyovipenda. Tafakari hii itakupa picha ya aina gani ya mtu wewe ulivyo, na kukusaidia kujipanga kuziba yale mapungufu, na wakati huo huo, utaweza kuangaza fursa zilizopo na unazoweza kuzitumia kutokana na 'ubora' ulionao.
Tafakari hii itakuwezesha pia kutambua kitu kiitwacho kwa kiingereza 'passion', yani mambo unayoyapendelea sana kufanya au kuwa hapo baadae. Umuhimu wa kutambua passion ni kwamba ukiweza kuwekeza muda katika passion yako inaweza kuwa sehemu nzuri ya kujijengea maisha yenye furaha. Kwani passion itakufanya ufanye jambo utalotaka kulifanya kwa ufanisi na pia hata ukikumbana na changamoto, hautokata tamaa kirahisi rahisi.
2. Mambo mazuri hayataki haraka
Kumbuka hao wote unaowaona wamefanikiwa kimaisha, mafanikio ambayo pengine unatamani uwe nayo, sio kwamba mafanikio hayo yalikuja kwa siku moja. Kuna maandalizi kadhaa waliyafanya, magumu waliyoyapitia mpaka kufika hapo walipofika.
Hii kwako ina maana kuwa ni lazima ujue kuna muda ni lazima uutumie kufanya maandalizi, inabidi utambue kuwa utakutana na magumu, ila hautakiwi kukata tamaa. Na zaidi sana ni lazima ujue bidii inahitajika. Hata hivyo bidii zako zitazaa matunda kwa haraka kama utatambua mapungufu yako mapema, na pia passion yako hasa ni ipi. Ukitambua mapungufu yako mfano una tatizo la lugha ya kiingereza, basi utafanyia kazi pungufu hilo ili uwe bora zaidi.

3.Utafiti ni muhimu sana
 Ni muhimu sana kuwa na taarifa sahihi kuhusu nini vinaweza kufanikisha  mipango yako na matarajio yako ya kimaisha. Mfano kama unatamani kufanya biashara, basi tafakari aina gani ya biashara, tafuta taarifa za kutosha kuhusu wateja wa biashara husika, kiasi cha mtaji , mbinu za kimasoko , n.k Vyote hivyo vitakuwezesha kujipanga kwa ufasaha ili kupunguza hasara na muda mrefu wa kufikia mafanikio.
Hii pia inahusika katika aina ya kazi unayotamani kufanya, je ni kwa kiwango gani utahitaji lugha ya kigeni, uwezo wa kutumia teknolojia mpya, kiwango cha elimu , n.k
4.Kubali kuwa tofauti
Wewe na yule mna historia tofauti za maisha, malezi tofauti, tabia tofauti, na hata uwezo wa kufikiri na hisia tofauti. Vyote hivi vinaweza kuchangia katika namna tofauti za kukabiliana na changamoto za kimaisha, na hata katika kupata fursa. Hivyo basi badala ya kuwaza kutaka kuwa kama fulani, tafakari nini wewe kama wewe unaweza kufanya, kiwango gani cha uvumilivu na juhudi kinahitajika ili kufikia malengo yako, na jitahidi kufanya unayotakiwa kufanya kwa juhudi.
Hakuna  'shortcuts' za mafanikio. Na mafanikio ya 'kulazimisha' hayawezi kukuletea furaha ya kweli maishani mwako.
Utakuja kugundua kuwa la msingi sana katika maisha ni kuwa na furaha na amani ya moyoni.
HITIMISHO
Kujitambua mapungufu yako na kuyarekebisha , halafu ukatambua pia mambo uliyo mzuri sana katika hayo, kisha ukazitumia fursa zinazoendana na hayo, kutakufanya ujiweke katika namna nzuri ya kupata dili za kuboresha maisha yako.
Hata hivyo kwakuwa mafanikio ni safari , unapaswa kujipanga kwa kuwa na taarifa sahihi, kuwa na bidii endelevu katika mambo ya msingi, na zaidi sana uweze kujitofautisha na wengine ili uweze kutambulika ubora wako, na hatimaye dili kali zije kwa ajili yako.

Sunday, 8 June 2014

Aliyoyasema ERIC SHIGONGO,Hakika yatakusaidia !!

  Erick Shigongo alianza hivi:

Kuzaliwa na kuishi duniani ni kutimiza kusudi la Mungu. Lipo kusudi ambalo Mungu analitaka ulitimize katika dunia hii nzuri yenye vitu vizuri vilivyoumbwa na Mungu. Hivyo ipo sababu ambayo ipo mbele za Mungu aliyokupa wewe uzaliwe mahali ulipo.

Wengi wetu tumezaliwa tukiwa na vipaji vingi na wenye uwezo mkubwa lakini wapo walioondoka katika ulimwengu huu bila ya wao kufahamu uwezo uliopo ndani yao. Kutokana na hali ya kutojitambua imewafanya kuhakiki ule usemi usemao kuwa:

'' Makaburini ndiko mahali walipolala watu wenye utajiri mkubwa ''. Utaji ambao walipokuwa hai hawakuujua wala kuutambua uwezo wao ambao kama wangeutambua basi leo hii ulimwengu ungekuwa ukishuhudia maajabu chanya kwa waliyoyafanya. Hivyo basi, kuondoka duniani bila kutimiza kusudi na wajibu wako kwa jamii yako ni kitu kibaya mno.

VITU MUHIMU VYA KUZINGATIA KWENDA KATIKA MAFANIKIO.

Kila jambo lenye misingi katika ulimwengu huu hufungamanishwa katika misingi muhimu. Ipo misingi ambayo ukiifuata na kuifanya itakupeleka katika kilindi cha mafanikio. Mambo yafuatayo tukiyatilia maanani basi tutafanikiwa:


1. KUJITAMBUA (Self Discovery)

Kujitambua huja baada ya kujichunguza. Maisha ya mwanadamu hukamilika pale mwanadamu huyo kama atakuwa na tabia ya kujichunguza. Utambuzi binafsi huwasaidia watu kujielewa kuwa yeye, wewe au mimi ni nani?. Utambuzi binafsi wa mtu ni silaha kwa mtu mwenyewe ambayo humlinda mtu huyo dhidi ya tabiri zenye kukatisha tamaa toka kwa watu ambao wapo kwa ajili ya kuwakatisha tamaa wengine.

   Mfano; utawasikia wakikueleza kuwa '' Huwezi kufanikiwa kwa sababu katika familia yenu hamna aliyefanikiwa''. Kitu muhimu cha kuweza kukabiliana na kauli za kukupuuza na kauli hasi za watu wa namna hii ni kujitambua. Daima elewa kuwa '' Dunia imejaa watu weledi wa kukosoa na kukatisha tamaa wenzao kila wanapoinuka. Usiwajali 'Inuka na kuanza sasa'!.

2. KANUNI.

Tambua kuwa ''Daima maisha ni kanuni''. Kanuni ambazo ukizitumia lazima uelekee katika mafanikio. Kanuni hizi hutumiwa pia na waliofanikiwa daima nikiwemo mimi (ERICK SHIGONGO). Hebu chunguza mfano huu '' Taarifa (info) + Kufanyia kazi = Mafanikio.

Hivyo, chochote unachokisikia ama kuzungumzwa ni taarifa: Taarifa ambazo ukizitumia lazima mabadiliko uyaone. Kanuni hizi si mpya bali tunazo katika maisha yetu ya kila siku. Hujulikana kama SHERIA ZA MAFANIKIO. Kanuni hizi ni za kweli. Nizungumzacho ni kweli kwa maana mahali hapa nilipo (Erick Shigongo) kuna watu wanao nijua, wanao ijua familia yangu siku za nyuma enzi za uchumi mbaya.
Niliamua kuzitumia kanuni hizi kwa kufanya maagizo (taarifa) hakika nimeyashuhudia na ninaendelea kushuhudia mabadiliko katika maisha yangu na familia yangu kwa ujumla. Nami leo kwa kulitimiza kusudi la Mungu ninasimama mbele yenu kuwaeleza kuwa jamii yetu inahitaji watu waliofanikiwa. Haitafaa kitu katika nchi hii watu wachache watafanikiwa ilihali wengi wao hawakufanikiwa. Ili nchi yetu (Tanzania) iweze kuendelea katika nyanja kiuchumi na kijamii tabaka la kati lazima lifanikiwe. Lazima liwe na uwezo mkubwa wa kiuchumi ambao utawezesha watu wengine kuajiriwa na kununua pia. Hivyo, nchi uliyopo ndio mahali sahihi kwako kufanikiwa. Unachopaswa kutenda ni wewe kujiamini. Kujiamini ni silaha katika kuelekea mafanikio. Kujiamini daima huleta mafanikio ambayo huanzia chini na si juu. Unapojiamini na kujenga hasira ya mafanikio ndani yako kuwa kwa nini yule alifanikiwa na mimi au wewe ushindwe. Kwa hiyo, kujiamini ni silaha ya kukupeleka katika mafanikio.

Tambua kuwa mtu awapo katika umaskini hupoteza kujiamini. Mfano halisi ni mimi Erick Shigongo, nikiwa darasa la tatu katika shule ya msingi Gedadi, Nyakato - Mwanza walikuwa wakiniita mjinga wa darasa. Hivyo, kutokana na umasikini ambao familia yetu ulipitia basi ulininyang'anya hali yangu yakujiamini darasani na hata nje ya darasa. Umasikini wa familia yetu ulinisababisha jina langu kupotea na kupewa jina la MADASA ambalo ni jina la Kisukuma lenye maana ya mtu mwenye kuvaa nguo zilizochanika.
Umasikini ulinidhalilisha, ulisababisha nipuuzwe mimi na wazazi wangu. Siku moja nikiwa na umri wa miaka kumi na minne nilikwenda kwa mara ya kwanza katika msiba wa rafiki yangu, ndipo niliposhuhudia wazazi wangu wakidhalilika kwa kukaa chini huku watoto wadogo wakiketi katika viti. Nakumbuka wazazi wangu walinifundisha kuwa kila nimuonapo mtu mkubwa amesimama nami nimeketi katika kiti au kigoda ni lazima nimpishe. Hali ile ilinitia uchungu moyoni nilimuuliza mama tukiwa nyumbani. Nililia mno kwa dharau ile kwa wazazi wangu. Mama alininyamazisha kwa sala ya baraka katika maisha yangu. Jifunzeni kuwafunza watoto wenu adabu njema. Hivyo, mambo hayo yalinitia hasira ya mafanikio kwa kauli za ndani yangu kuwa ''Nitamfanya kila mtu kuwa na adabu kwa wazazi wangu''.

3. KUWA NA UPENDO WA DHATI.

Upendo ni nguzo kuu katika maisha. Kuwa na upendo kwa watu wote, nchi yako na uudhihirishe upendo wako. Usiwe na kisasi kwani kisasi ni cha Mungu. Kwani kawaida ya Mungu kuwaleta mbele yako wale wote waliokutenda vibaya baada ya kufanikiwa ili uamue kuwasamehe au la.

'' Nakumbuka kijana mmoja aliwahi kufukuzwa kazi na mkuu wake kwa fitina ambayo ilitokana na utendaji kazi mzuri na elimu aliyokuwa nayo yule kijana. Hivyo, mkuu huyo alimfukuza kazi kijana yule kwa dhihaka na matusi. Baada ya miaka kupita naye alifukuzwa kazi akaanza kutafuta ofisi ya kukodi ili afungue ofisi yake. Siku moja alijikuta katika jengo refu ambalo alikuwa akimuuliza mhaziri (secretary) mara kijana yule aliyemfukuza alipita na akamuona kijana akipita. Alimuuliza mhaziri, huyu ni nani hapa? (kwa jazba) mhaziri alimjibu kwa upole: ''Huyu ndiye mkuu hapa na ndiye mwenye jengo hili''. Jamaa aliingia ofisini mikono ameweka nyuma alikwenda kumtaka radhi na kumwambia: ''Yaliyopita si ndwele tugange yajayo''. Hivyo, upendo kwa watu wote ni mojawapo ya njia katika mafanikio.

4. JIVUNIE KITU ULICHO NACHO.

Mtu bora katika dunia ni yule anayekionea fahari kitu alichonacho hata kama ni kikubwa au kidogo.

5. Tambua kuwa mafanikio yako katika maisha yatokane na hasira ya kufanikiwa, hivyo mateso au vitu ulivyopitia ndio nguvu itakayokusukuma kubadili maisha yako. Pia amini kuwa Mungu hashindwi kukuinua. Elewa kuwa Mungu anapomnyanyua mtu anamnyanyua kwa makusudi yake si kwa sababu wewe au mtu huyo ni mwema, la hasha! ni kwa sababu tu Mungu wetu ni mwema na ni mwaminifu.

Amini maisha unayoishi sasa ya taabu ni ya kitambo tu kwani yapo maisha mazuri mbeleni. Katika kipindi cha mwanzo lazima uwe mpole na mnyenyekevu mbele za Mungu. Mungu anaruhusu upite katika shida ili uwe na mizizi iliyokomaa, kimbunga kitakapokuja usitetereke wala kung'oka. Pia usikubali mwanao aitwe majina na wengine, jifunze kuwaeleza watoto wako habari za watu waliofanikiwa na umweleze uwezo uliomo ndani yake katika kuleta mabadiliko ya kimafanikio katika maisha.
Usiridhike na maisha uliyo nayo sasa piga hatua ubadilishe maisha na uwe na furaha.

HATUA ZA MAFANIKIO.

Ili tuweze kufikia mafanikio yatupasa kufanya na kujua kuwa:

UCHAGUZI > Mambo yote yamefichwa katika kuchagua. Kila unachokichagua ndicho upewacho. Kuna aina mbili za uchaguzi yaani uchaguzi bora na uchaguzi mbaya. Chaguzi bora matunda yake ni bora na chaguzi mbaya matunda yake ni mabaya. Hivyo jifunze kuchagua vilivyo bora katika maisha yako. Watu wengi watesekao sasa na wale walioteseka kale sababu kuu ya mateso yao walichagua vibaya. Ukichagua vyema utapuuza kubezwa. Hali ya kutojiamini itatoweka na utachagua kujiamini katika kila jambo utakalolifanya. Achana na kasumba mbaya kuwa wewe huwezi mbele za mzungu kwa sababu yeye ni mweupe au wewe ni mweusi. Achana na maneno ya uongo yanayosemwa juu yako.

Jifunze kutoka kwa kila mtu hata kama ni mjinga.

Usimruhusu mtu akuamulie kesho yako. Elewa kuwa kesho ni yako na Mungu wako, jifunze si kila kitu unachotaka kukifanya ni lazima umwambie mtu.

* Kuwa tayari kukubaliana na changamoto (Calculated Risk). Katika kuelekea mafanikio uwe tayari kukubaliana na changamoto zake. Pia epuka kuchukua muda mrefu katika kuandaa mambo yako. (Do be smart). Mpango mkakati si muhimu sana kwa sababu haukuelezi mambo mengi ya ziada.

* Chagua kuweka lengo katika maisha. Lazima uingie na lengo katika maisha yako. Ingia katika maisha ukijua wapi unakoelekea na lengo ndilo litakalokujenga wewe. Kama unataka pesa jiulize ni shilingi ngapi? Zije lini, tenga muda wa utekelezaji wa lengo lako.

-Jifunze kuweka lengo kubwa usiangalie uwezo ulionao wakati unapanga lengo lako. Achana na malengo madogo madogo. Elewa kuwa kama unataka kuwa si mtu wa kawaida basi malengo yako yawe ni makubwa. Tengeneza lengo kubwa kisha ligawe katika sehemu ndogo ndogo.
-Daima wenye malengo ndio wenye kuteseka.

* Chagua kupanga mipango.
Ukichagua lengo bila kupanga huwezi kufanikiwa. Tazama ulicho nacho na uanze nacho. Anza na ulicho nacho. Mungu hawezi kukupa wazo halafu akunyime msaada ila huwezi kupewa msaada na Mungu bila ya kuanza. Katika maisha ya kuanza mafanikio unahitaji mambo makuu matatu ambayo ni WAZO, WATU na FEDHA. Lakini vitu hivi vyote huwa haviji vyote kwa pamoja. Wanadamu ni wataalamu sana katika kuwaza lakini utekelezaji hakuna. Elewa kuwa kila kitu kinachofanyika duniani ni Mungu anafanya kupitia watu wake, weka mawazo yako ardhini ili yaonekane.
-Chagua ushindi kwa kila wazo unalopewa.

* Chagua Kutenda.
Ondoa woga na ufuate malengo yako uyatimize. Achana na kuogopa kufanya kuwa ukifanya ukishindwa utachekwa tambua kuwa hata usipofanya utachekwa tu. Fanya mpaka mwisho wako na Mungu atakuletea watu wa kukusaidia.
-Kuwa king'ang'anizi katika kutimiza malengo yako.
-Tambua kuwa kuna watu wana fedha zako ila anza kufanya ili ukutane nao

* Chagua kuwa mvumilivu.
Chagua kuwa mvumilivu, maisha ya mafanikio ya muda mfupi sio mazuri. Ukubali au kuwa mvumilivu hata unapokutana na changamoto. Maana mvumilivu hula mbivu daima, mafanikio yamo katika uvumilivu.

* Chagua kuwa na nidhamu ya pesa na wakati.
Hakuna mafanikio duniani bila kuwa na nidhamu ya muda na pesa. Elewa kuwa kila mtu duniani ana thamani, tambua kuwa kila unachokifanya kina thamani yake katika muda. Itambue thamani yako kwani kila mmoja ana thamani. Jiulize swali hili kuwa ''Unautumiaje muda wako/''. Watu wengi wanahusisha giza na usingizi bila kujua kuwa ni vitu viwili tofauti. Usiku pia ni muda mzuri wa kuweza kufanya jambo ambalo litakuingizia kipato. Tumia saa 24 kutengeneza fedha wewe mwenyewe au kupitia wengine (kuwaajiri).
-Heshimu fedha yako kwa kuudhibiti mkono wako. Jifunze tabia ya kuwa na nidhamu katika fedha hata kama huna jilazimishe. Wekeza fedha yako katika vyanzo vingine vya mapato.

* Chagua marafiki sahihi.
Uchaguzi wa marafiki walio sahihi watakupeleka mbele. Achana na marafiki wanaokuletea habari za matumizi ya pesa. Achana na rafiki ambaye unampa tu yeye hatoi. Maana urafiki ni kutoa na kupokea.

* Chagua watu unaotaka kufanana nao.
Chagua watu waliofanikiwa au unayemtamani kuwa kama yeye katika mafanikio.

* Chagua kujifunza.
Elewa kuwa kujifunza hakuna mwisho. Jifunze kila siku bila kusimama. Achana na tabia ya kuacha kusoma baada ya kumaliza shule au chuo. Soma vitabu mbalimbali vya ndani na nje ya taaluma yako kwa sababu hujui kitakachokuja kukuweka huru kifedha.

* Chagua kusaidia jamii baada ya mafanikio.
Tuna kila sababu ya kuwasaidia wasiojiweza. Msaidie mtu mwingine ainuke, hutafirisika.

MWISHO

Sunday, 4 May 2014

unaweza kuacha kazi ili ujiajiri

HUENDA wengi wakashtushwa na mada hii lakini ni ukweli usiopingika kuwa kuiajiri ni bora kuliko kuajiriwa. Kama wewe umeajiriwa, unaweza kuacha kazi na kujiajiri mwenyewe. Ni rahisi na kamwe hutajutia uamuzi wako.
Wengine hufananisha suala la kuacha kazi na tukio la kuruka kwenye dirisha la ndege ukiwa na parachuti ukitegemea kama litafunguka ili utue salama. Kama utajiandaa vyema, utakuwa sawasawa na mtu ambaye ameelekezwa vizuri namna ya kutumia parachute na amejiandaa barabara kiakili na kihisia.
Utafiti unaonyesha kuwa katika kila biashara zinazoanzishwa, asilimia 95 huanguka ndani ya miaka mitano na 5% huendelea. Lakini baada ya hapo asilimia 95% ya biashara ya asilimia hii huanguka ndani ya miaka 5 ifuatayo. Kwa nini kiwango cha biashara kuanguka ni kikubwa hivi? Kwa nini watu wengi huwa wanafilisika? Zifuatazo ni baadhi ya sababu:
1. Mjasiriamali kukosa uzoefu wa biashara
2. Mjasiriamali kukosa ujuzi na maarifa ya masoko
3. Kukosa nidhamu ya pesa
4. Kukosa mtaji
5. Mauzo kuwa chini
6. Kushindwa kuendana na baadhi ya wafanyakazi wake
7. Kuchukua mkopo mwingi bila matumizi sahihi
8. Kukosa stadi za mafanikio katika ujasiriamali
9. Kukosa msukumo binafsi wa kufanya mambo sahihi
10. Kujaribu kufanya biashara nyingi sana au mambo mengi ambayo yote yanahitaji muda na umakini (lack of focus)
11. Kukosa ndoto na shauku ya kufanikiwa
12. Magonjwa na afya mbovu
13. Tabia ya kuahirisha mambo mra kwa mara
14. Kukata tamaa kwa urahisi mambo yanapoonekana magumu
15. Mtazamo hasi (negative mental attitude)
16. Hali ya kutaka kitu bila kitu.
17. Marafiki au washirika wasio sahihi katika biashara yako (mkeo au mumeo aweza kuwa kikwazo)
18. Hofu na kutokuthubu
19. Kushindwa kufikiri kwa makini na kupenda kukisia mara kwa mara.
NATAKA KUACHA KAZI, NIFANYE BIASHARA GANI?
Mara nyingi hilo ndio swali ambalo huwa ninaulizwa sana. Watu hunipigia simu wakisema kuwa wamenisikia kwenye vipindi vyangu vya ujasiriamali (huwa naendesha vipindi vya redio vya ujasiriamali) na hivyo huomba ushauri wa waanze vipi na wafanye biashara gani
Hilo ndiyo swali la muhimu sana kwa mtu anayetaka kuwa mjasiriamali na linaweza kumsaidia mtu kupata majibu sahihi ya kitu atakachokifanya na kumletea mafanikio maishani.
Watu wengi wakiulizwa ni biashara gani inaweza kukupatia fedha kwa urahisi, hujibu kwa kuangalia watu waliofanikiwa kupitia biashara mbalimbali na kuzitaja biashara hizo kama ndiyo zina faida kubwa. Ukweli ni kwamba biashara yeyote inaweza kufanikiwa ikiwa itapata wateja wengi wakutosha. Hivyo suala la msingi, sio biashara gani ya muhimu, bali ni vigezo gani vya msingi.
KABLA HUJAACHA KAZI ZINGATIA YAFUATAYO:
 • Chunguza siri za biashara zinazofanikiwa na mifumo iliyopo nyuma yake. Jaribu kuziangalia biashara za Wahindi na Waarabu zinazofanywa. Watu wengi huwa na wazo la bidhaa ya kuuza au hata kutengeneza kama vile mshumaa, rangi, shampoo nk lakini mara nyingi huwa hawana ujuzi wa kutengeneza mfumo mzuri wa uletaji wa faida.
 • Pata mlezi au mshauri (Mentor) atakayekusaidia katika safari ya ujasiriamali. Neno mentor linamaanisha mtu ambaye amefanikiwa kwenye jambo fulani na ana uwezo wa kuwasaidia/kuwaelekeza watu wengine wafanikiwe kama yeye.
 • Fanya kazi kwenye biashara ya mtu aliyefanikiwa na ambaye unataka kuja kuwa kama yeye. Wakati mwingine, njia ya mkato ya kujifunza biashara ni kukubali kutumika chini ya mtu mwingine ili ujionee moja kwa moja uendeshaji wa biashara kabla hujaamua kuingia moja kwa moja.
 • Jenga tabia ya kuwauliza maswali ya msingi wajasiriamali waliofanikiwa. Kila unapopata nafasi ya kuwa na mtu tajiri, jipe moyo mara kwa mara halafu uliza swali hili: “Je siri ya mafanikio yako ni nini?”Utashangaa jinsi ambavyo watu wengi si wachoyo wa siri zao za mafanikio ili mradi tu uulize katika mazingira mazuri yenye heshima na hekima.
5. Jijengee uwezo wa kuuza. Uwezo wa kuwashawishi watu waweze kununua bidhaa yako au kutumia huduma yako ndiyo uweze kusimama katika ujasiriamali.

Wednesday, 26 March 2014

TUNAJITAHIDI KWA KIWANGO GANI?

Wakati tunaelekea kwenye maadhimishi ya kuzaliwa RAJOMBO INVESTMENT tarehe 3 April 2013 tunaomba kujua maoni yako katika post zetu tunazozipost Facebook na kwenye blog yetu hii !!
Maoni yako ni Muhimu !!

Thursday, 13 March 2014

Mbinu 13 na rahisi za kupata ujasiri kimafanikio


.
1. Kutoshindana na waliofanikiwa.

Daima mtu ahakikishe anawafanya waliofanikiwa wajione wapo juu. Kama mtu anataka kuwashangaza basi asionyeshe ujuzi wake wote.
Kuwapa waliofanikiwa heshima yao kutamfanya mtu apate msaada na hatimaye afikie kiwango cha juu bila ya kupata tabu nyingi.

Mfano, mtu asishindane na mwajiri wake ili kuonekana anajua sana; asishindane na tajiri katika matumizi hususani mazingira ya kijamii kama baa, misiba n.k. Waliofanikiwa hutafsiri kitendo cha kushindana kama kuonyesha kiburi au maskini jeuri.

2. Kutoamini sana marafiki.

Mtu awe makini 'anapojamiiana' na marafiki au watu wa karibu. Watu wa karibu huwa wasaliti na huvujisha siri kwa wapinzani. Mtu aogope marafiki zaidi ya maadui, ikibidi awape nafasi wale anaohisi ni wapinzani. Ilkiwa mtu hana wapinzani, ajitahidi kuwatafuta. Mtu ajifunze jinsi ya kutumia wapinzani kimafanikio, si kuwaamini marafiki muda wote.

3. Kuficha malengo.

Mtu afiche matarajio yake au dhamira za matendo yake. Kuweka malengo hadharani huwafanya watu wenye nia mbaya kujipanga na kuvuruga malengo husika. Mtu akinge malengo yake na ikiwa yatagundulika iwe nyakati za mwisho; nyakati ambazo wapinzani hawawezi kuweka vikwazo.

4. Kutumia wasidizi.

Kufankiwa kwa mtu kunategemea mchango anaoupata kutoka kwa wale wanaomzunguka (mazingira na marafiki). Mtu atumie busara, ujuzi na maarifa ya wale anaofanya nao kazi ili kusonga mbele. Msaada haupunguzi tu nguvu, bali pia huongeza ufanisi na kuimarisha urafiki. Mtu hupata fadhila kutoka kwa wasaidizi wake, ndipo jamii husika. Hivyo, mtu awaachie watu wengine yale wanayoweza kufanya kwa ufanisi.

5. Kushinda kupitia matendo.

Ushindi mtu anaopata kupitia maneno haufai kitu! Mtu asishindane juu ya uwezo wake kwa maneno bali, aache matendo yaongee. Ushindi makini ni ule mtu anaoupata kupitia matendo yake, na si kwa wingi wa maneno. Uhalisia wa matendo huonyesha umakini wa mtu kwa jamii inayomzunguika. Mtu husifiwa kwa kadiri ya juhudi zake za hali na mali kutatua changamoto zinazomsonga, si kwa kupiga domo.

6. Kujenga utegemezi.

Ili mtu kujua umuhimu wake katika jamii anapswa kjua kwa kiasi gani mchango wake unahitajika. Mtu ajenge mazingira ya kutegemewa; kutegemewa kuleta furaha au ustawi katika mazingira yanayomzunguka.

Ili kfanya hivyo, mtu asitoe mbinu zote alizo nazo juu ya kitu fulani. Kutegemewa humwezesha mtu 'kuuza' kile alichonacho kwa mafanikio yake na ya jamii yake. Hivyo, mtu ajue wakatigani wa kuficha huduma yake, wakati gani wa ktoa kidogo na wakati gani wa kutaka watu wailipie.

7. kutenda kama mpelelezi.

Ni muhimu sana mtu kujua juu ya wapinzani wake. Mtu atumie marafiki (wapambe) ili kupata taarifa muhimu juu ya udhaifu na uwezo wa wapinzani wake. Kufanya hivyo kutamwezesha mtu kupanga mipango ya kiulinzi na ambayo haitazimika katika safari yake ya mafanikio. Kupata taarifa kunafanikishwa kwa kuuliza maswali rahisi, kuuliza kwa njia ya upole na kwa kutumia mifano. Kila wakati ni fasaha kwa upelelezi.

8. Kuwafahamu watu wa karibu.

katika mazingira yoyote yale kuna watu wa aina nyingi. Watu hutofautiana kiimani, kitabia, kimalengo, kiutendaji n.k. Watu wa karibu ndio wanaotoa au kufanikisha kotoa ushindani katika mazingira yasiyotegemewa. Watu wengi, tena wa karibu ni kama mbwa mwitu. Ili kufahamu watu wa karibu, mtu atafakari kwa kina misingi mikuu ya urafiki huku akibadilisha muonekano, kutoa changamoto kwa walengwa n.k. Pindi mtu anapofanya yote hayo atazame mwitikio ya walengwa.

9. Kuwa na dira.

Dira humwezesha mtu kufika kule anakotaka. Mtu anapaswa kuweka malengo juu ya kule anakotaka kufika baada ya muda fulani pia, changamoto azazohisi zitamkumba sambamba na suluhu sahihi. Kwa kuwa na malengo haitakuwa ngumu sana kukabiliana na vikwazo mtu awapo safarini. Watu wengi huweka malengo huku wakisahau au kupuuzia adha zinazoweza kuwakumba au zilizowakumba watu wengine waliokuwa na malengo kama yao.

10. Kujikuza.

Mtu asipokee na kukubali sifa 'chafu' anazopewa na jamii. Mtu anapaswa kujikuza kwa kuvaa utambulisho mpya; ambao unavuta umakini na hauiudhi jamii yake. Mtu anapaswa kutawala taswira yale, si taswira yake ktawaliwa na nguvu kutoka nje. Kujikiza kwa jitihada za mtu huleta taswira ya kudumu, na ambayo italeta uaminifu wa kweli na kukubalika katika jamii.

11. kuwa na shabaha.

Mtu anapaswa kuelekeza nguvu na jitihada kwa yale anayoamini yataleta matunda mazuri. Mtu awe makini kutunza au kutenga nguvu za ziada kwa ajili ya changamoto. Ili kutokata tamaa, mtu anapswa kuwa na wadu (watu wa karibu) wenye uwazo tofauti tafauti kama vile madaktari, wafanya biashara, waalimu, viongozi wa dini, wazee wenye busara n.k

12. Kujirudisha nyuma.

Kama mtu akiona changamoto zitamzidi siku a usoni, huku mbinu alizo nazo au mikakati yake itakuwa dhaifu ahairishe 'pambano'. Kurudi nyuma kutampa mtu nafasi ya kujipanga kwa kukusanya nguvu na 'kuusoma mchezo zaidi'. Mtu asikubali kuangushwa kabisa na changamoto ndipo ajiandae kuinuka. Ni vigumu sana mtu kuamka baada ya kushambuliwa na kuangamizwa na chahangamoto za kimaisha.

13. Kutojitenga.

Kujitenga na jamii au marafiki ni hatari sana! Kwani ulimwengu ni tambara bovu na uumejaa wapinzani kila kona. Inapasa mtu kujiundia ngome ya ulinzi lakini, si kwa kujitenga. Kujitenga hupunguza mawasiliano na watu na pia uwezekano wa kupata misaada ya hali na mali. Kwa mfano, kuna uwezekano mkubwa wa kukosa habari, ushauri, vitendea kazi n.k. Vitu ambavyo ni muhimu kufikia mafanikio.

Friday, 31 January 2014

Umekosa ajira au mtaji?.Fanya mambo haya saba kubadilisha maisha yako !!




Makala hii inalenga kuibua tafakari ya namna bora ya kutafuta ajira na kuanzisha shughuli binafsi za kijasiriamali. Ingawa ni kweli kuwa kuhitimu ngazi fulani fulani za elimu ni jambo la msingi katika kupata ajira au kuwa na shughuli imara za kijasiriamali, wengi wamejikuta ngazi zao za elimu haziwasaidii kukabiliana na changamoto za ajira na ujasiriamali.
1. Boresha uwezo wako wa ufasaha wa lugha : Lugha ndio msingi mkuu wa mawasiliano. Jikite vema katika Kiswahili fasaha, na kiingereza kinachofuata kanuni sahihi katika kuongea na kuandika. Haijalishi una kiwango gani cha elimu, fanya bidii kuboresha uwezo wako wa kuandika vema na kuongea. Tumia hata internet kutafuta namna bora za kuboresha uwezo wako wa kuongea na kuandika kwani ‘broken’ english haitokufikisha popote, na Kiswahili kisichofuata kanuni hakitokufanya watu wakuchulie ‘serious’ katika maamuzi yao ya kufanya kazi nawe, iwe kibiashara au kiajira.
2. Jikite katika ujuzi fulani: Kama unataka kuitegemea elimu yako kuzalisha huduma au bidhaa fulani, ni lazima basi uwe kweli na ujuzi wa uhakika katika jambo fulani, na  sio tuu kuwa na cheti. Tafakari kwa umakini katika vyeti ulivyo navyo, ni mambo gani haswa unaweza kuyafanya kwa ufasaha, jikite katika hayo, ili kuwa na ujuzi imara utakaokupa heshima na kukubalika mbele ya wateja wako watarajiwa. Zaidi sana kumbuka, unaweza kujifunza ujuzi mpya usiokuwepo katika vyeti vyako.
3. Jitangaze : Kupitia mtandao wako, kupitia mikutano mbalimbali unayohudhuria iwe ya kifamilia, kidini, marafiki au vikundi vingine, hakikisha watu wanatambua uwepo wako , na kuwa wanajua kuwa unao ujuzi fulani. Zaidi sana sio tuu wajue unao ujuzi fulani, bali wajue pia kazi ulizokwisha fanya kupitia ujuzi fulani ulio nao. Watambue pia kuwa upo unapatikana kama utahitajika kwa ajira au kibiashara. Mitandao kama Facebook, inaweza pia kutumika kujieleza uwezo wako.
4. Jenga mtandao wa watu mbalimbali: Kuwa karibu na watu mbalimbali ili uweze kujifunza mengi toka kwao, na pia watu hao wanaweza kuwa wa msaada mkubwa kwako kama wateja wako, au wasambaji wa bidhaa fulani unazohitaji. Pia watu katika mtandao wako wanaweza kukusaidia kupata mtaji wa kuanzia ujasiriamali wako. Hata hivyo kumbuka, watu wamsingi katika kujenga nao mtandao wanahitaji kukutambua wewe kama mtu muhimu kwao pia, hivyo jiweke kama mtu muhimu kwa kuonyesha uadilifu, ujuzi wako, na heshima kwa wengine. 
5. Kuwa mbunifu: Tambua kuwa kinachowafanya watu kununua bidhaa fulani ni kwakuwa wanaamini bidhaa hiyo itakidhi hitaji lao. Hivyo basi tumia muda wako kuangalia matatizo au changamoto katika jamii na jinsi unavyoweza kuleta suluhu za changamoto hizo. Sio lazima uzalishe bidhaa mpya kabisa, hata kusaidia kuleta huduma adimu sehemu fulani, kusaidia kuboresha utendaji kazi wa watu kwa huduma za kiakili unazoweza kutoa kama ushauri, ni moja ya ubunifu unaoweza kufanya. Kumbuka ubunifu si jambo la haraka, unahitaji muda kusoma mazingira, fani na watu, kisha utafakari namna unavyoweza kutumia ufahamu wako wa mazingira, ujuzi mbalimnbali, na tabia za watu, ili kuleta huduma au bidhaa itakayohitajika na watu.
6. Fikra sahihi:  Kila mmoja wetu ana njia ya kipekee ya kufikia mafanikio yake maishani. Ingawaje ni kweli kuwa ajira na biashara zinatuingizia kipato cha kujikwamua kimaisha, hakuna kanuni moja ya namna gani utaingia katika ajira au biashara ili ufanikiwe kama fulani. Hivyo basi , usijilinganishe na watu wengine, kubali kuwa maisha yako ni ya kipekee, fikiria hali uliyo nayo kuwa ni ya kipekee na inahitaji suluhu ya kipekee. Hivyo tafuta njia yako ya kipekee ya kujiajiri kwa kuangalia hobbies zako, mtandao wako,  ujuzi wako n.k. Pengine hata kutokupata kwako kazi ni kwa sababu unawaza kupata ajira kama fulani na fulani walivyopata, au unawaza aina fulani ya kazi ndiyo ‘itakayokutoa’ kimaisha. Kumbuka kuna baadhi ya watu wana degree mbili na hawana kazi nzuri zaidi ya watu wenye degree moja, na kuna watu waliishia darasa la saba tuu, ila wana kipato kizuri na maisha bora.
7. Ota kwa usahihi na ujiamini: Hata kama unahisi hali yako kimaisha sio nzuri, bado unahitaji kuweka picha kubwa ya maisha yaliyo bora hapo baadae. Kuota sahihi ni kufikiria kwa umakini nini hasa unapenda kufanya, nini hasa unatamani yawe mafanikio yako, na zaidi sana kuota huku kunakuwezesha kujiona kabisa umefikia hali husika unayoitamani kwani unaamini na kujiamini kuwa zipo njia za kufikia huko. Kuota na kujiamini ni muhimu kwani ndiko sikuzote kutakako kusukuma kuendelea na unachofanya hata kama unapitia magumu, ndio wahenga walisema “palipo na nia, pana njia”.  Ukiota vema na ukajiamini, hautokaa tuu bure bure, ukilalamika ajira ngumu, au hauna mtaji, badala yake utatafuta mbinu za ziada, na kuwa mbunifu kwakuwa unakitu kinachokusuma kukifikia katika maisha yako, na hasa ndoto hiyo ikiwa inajumuisha kuleta mabadiliko katika maisha sio tuu, mabadiliko kwa maisha yako peke yako, bali kwa jamii pia.